Hajib aipa ushindi Yanga Ligi Kuu, Yaipiga 1-0 Ndanda

Hajib aipa ushindi Yanga Ligi Kuu, Yaipiga 1-0 Ndanda


YANGA SC imepata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Ndanda FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.

Shukrani kwake, mfungaji wa bao hilo pekee, mshambuliaji mpya kutoka kwa mahasimu, Simba SC, Ibrahim Hajib Migomba aliyefunga dakika ya 34 baada ya kazi nzuri ya beki wa kati, Kevin Patrick Yondan.

Beki wa kulia, Juma Abdul Mnyamani alimuanzishia kona fupi Yondan, ambaye alijitengeneza na kutia krosi maridadi iliyounganishwa nyavuni na Hajib kwa staili ya kujipinda maarufu kama baiskeli.

Lakini Yanga itamkosa kiungo wake mpya, Mkongo Papy Kabamba Tshishimbi katika mchezo wake ujao na Mtibwa Sugar Septemba 30, baada ya kuonyeshwa kadi ya njano na refa Jeonisya Rukyaa wa Kagera leo, ambayo inakuwa kadi yake ya tatu mfululizo.

Pamoja na ushindi huo, lakini Yanga hawakuwa katika mchezo mwepesi, kwani Ndanda FC walicheza vizuri na kutengeneza nafasi ambazo hata hivyo, walishindwa kuzitumia.

Muda mrefu kipindi cha pili, mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Ngoma alicheza akiwa anachechemea kabla ya kutolewa dakika mbili za mwisho akimpisha Emmanuel Martin.
Yanga ilifunguka na kupeleka mashambulizi mengi mfululizo langoni mwa Ndanda dakika 15 kuelekea mwisho wa mchezo.

Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Youthe Rostand, Juma Abdul, Gardiel Michael, Andrew Vincent, Kevin Yondan, Papy Kabamba Tshishimbi, Obrey Chirwa, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma/Emmanuel Martin dk89, Raphael Daudi na Ibrahim Hajib/Geofrey Mwashiuya dk75.

Ndanda FC; Jeremiah Kasubi, William Lucian ‘Gallas’, Ayoub Masoud, Hamad Waziri, Hemed Khoja, Rajab Zahir/Kelvin Friday dk47, Jacob Massawe, Majid Bakari, Omary Mponda, Jabir Aziz na Nassor Kapama/Ophen Francis dk58.

Post a Comment

0 Comments