Kichuya awatoa hofu Simba

Kichuya awatoa hofu Simba


SHIZA KICHUYA.

WINGA wa Simba inayodhaminiwa na Kampuni ya Kubashiri Matokeo ya SportPesa, Shiza Kichuya, amewatoa hofu mashabiki wa timu hiyo kwa kusema anaendelea vizuri baada ya kuumia kwenye mchezo uliopita dhidi ya Mbao FC.

Kichuya aliumia na kulazimika kutoka nje kwenye mchezo huo uliochezwa Alhamisi iliyopita katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Akizungumza na gazeti hili jana, Kichuya alisema anaendelea vizuri na hatarajii kukaa nje kwa muda mrefu.

"Mimi naendelea vizuri, mashabiki wala wasiwe na hofu na mimi," alisema Kichuya.

Aidha, nyota huyo alisema kuwa sare waliyoipata kwenye mchezo dhidi ya Mbao, haijawavunja moyo na badala yake imewapa morali ya kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye mchezo wao unaofuata.

"Matokeo yale tumeyachukulia kama changamoto kwetu kuhakikisha tunashinda mchezo ujao na kuhakikisha tunajipanga vizuri kwa michezo ya ugenini," alisema Kichuya.

Simba inajiandaa kucheza na Stand United Jumapili ijayo kwenye Uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga.

Mchezo huo utakuwa wa pili kwa Simba kucheza ugenini baada ya sare yao dhidi ya Mbao ambao ulikuwa wa kwanza kucheza nje ya Dar es Salaam msimu huu.

Post a Comment

0 Comments