Zabibu Kiba afunga ndoa na Mwanasoka Abdi Banda

Zabibu Kiba afunga ndoa na Mwanasoka Abdi Banda


Baada ya miezi kadhaa kupita tangu nyota wa Bongofleva Alikiba aingie kwenye ndoa, hatimaye amefanikisha ndoa ya mdogo wake wa kike aitwaye Zabibu Kiba ambaye ameolewa na mwanasoka Abdi Banda alfajiri ya leo Agosti 1.

Ndoa hiyo ya mchezaji wa zamani wa Simba SC na Coastal Union ambaye kwasasa anachezea Baroka FC ya Afrika Kusini, imefungwa kwenye msikiti wa Masjid Ahmadi Al Maseeid uliopo Tabata-Sanene, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taratibu za dini ya Kiislamu, Alikiba ametekeleza jambo hilo la kumuozesha dada yake kwa Banda baada ya kupata ridhaa kutoka kwa dada yake Zabibu Kiba.

Ujio wa ndoa ya Banda na Zabibu uliripotiwa mapema baada ya Alikiba na mdogo wake Abdu Kiba kuoa kwa kupishana siku chache tu huku sherehe ya harusi yao ikifanyika siku moja. Banda aliwatakia kheri shemeji zake kwa kuandika, ''Hongera sana @officialalikiba anafuata @officialabdukibaa halafu.. kila la kheri katika kutimiza jambo muhimu sana kwenye dini yetu''.


Alikiba (kushoto) akitoa mkono kwa Abdi Banda ikiwa ni ishara ya kufungisha ndoa.

Ndoa hiyo imehudhuriwa na watu mbalimbali akiwemo Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu. Waziri Ummy ni miongoni mwa watu wa karibu wa mchezaji Abdi Banda.

Post a Comment

0 Comments