Vijana washauriwa wasipishane na fursa kwenda nje ya nchi na kuwaachia wageni

Vijana washauriwa wasipishane na fursa kwenda nje ya nchi na kuwaachia wageni



VIJANA wametakiwa wasipishane na fursa kwa kwenda nchi ya nchi kuzitafuta wakati wenzao wa nchi hizo wakija kunufaika nazo hapa nchini.

Rai hiyo imetolewa na Kamishina wa Polisi Mussa Ali Mussa wakati akihutubia kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye Maadhimisho ya Siku ya Amani Duniani-Tanzania yaliyofanyika leo Viwanja vya Mwembe Yanga jijini Dar es Salaam.

"Vijana acheni mipango ya kwenda kuzitafuta fursa nje ya nchi kwani wenzenu kutoka nchi hizo wamekuwa wakija kunufaika nazo hapa nchini" alisema Mussa. Alisema serikali imeweka mazingira mazuri hivyo ni vizuri hali hiyo ikatumika kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo hasa katika wakati huu nchi ikiingia katika uchumi wa viwanda.

Aliwataka wazazi na walezi kutoa malezi bora kwa watoto wao ili kuwaepusha kujiingiza katika makundi yasiofaa.Katika hatua nyingine Kamishna Mussa alisema amani ya nchi itadumishwa na kila mtu na kuwa watu waondoe dhana ya kuwa amani hiyo italetwa na vyombo vya dola ikiwemo polisi.

Alisema suala la amani si la mtu mmoja bali ni la kila mtu jeshi la polisi kazi yake ni kuilinda na kumkamata mtu yeyote anayeonekana kusababisha viashiria vya kutoweka kwa amani hiyo.Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa na Mkuu wa Shirika la UN linaloshughulikia wahamiaji la IOM, Dk. Quasim Sufi alisema amani ni jambo la muhimu kwa nchi na mustakari wa maendeleo.

Alisema bila ya amani hakuna kitu kitakacho weza kufanyika na ndio maana UN imekuwa ikisisitiza amani duniani kote.Sheikh Hemed Bin Jalala alisema amani ndiyo msingi wa dini zote ya kiislam na kikristo na kuwa amani haipaswi kuchezewa kwani ndio neema tuliyopewa na mwenyezi mungu.

Jalala alisema amani ni msingi wa dini uliojengwa kiimani na kutakiwa kuihubiri na kuwa wale wanaohubiri vita na machafuko wanatoka katika dini ya mashetani.Afisa Habari Kitemgo Cha Habari cha Umoja wa Mataifa-UNIC, Stella Vuzo aliwataka vijana kuendelea kuidumisha amani iliyopo nchini kwani wao ndio rahisi kurubuniwa kutokana na kuwa wengi.

"Katika maadhimisho ya siku ya amani duniani tunapenda kuwashirikisha vijana kutokana na wingi na umuhimu wao katika kutunza amani" alisema Vuzo.Alisema vijana watumie fursa ya amani iliyopo nchini katika kufanya shughuli zao za maendeleo badala ya kukaa bure.

Vuzo alisema Kauli Mbiu ya maadhimisho hayo mwaka huu ni " Pamoja Katika Kudumisha Amani: Heshima, Usalama na Utu kwa wote"

Maadhimisho hayo yameandaliwa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na taasisi mbalimbali kama Global Peace Tanzania, Global Network of Religions for Children- GNRC, Chama cha Scout Tanzania, Asasi ya Vijana wa Umoja wa mataifa YUNA Tanzania, wanafunzi na wananchi.

Post a Comment

0 Comments