ALIYESABABISHA HASARA YA TSH BILIONI 1.16 KAFIKISHWA TENA MAHAKAMANI LEO

ALIYESABABISHA HASARA YA TSH BILIONI 1.16 KAFIKISHWA TENA MAHAKAMANI LEO



Upande wa Utetezi katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia Serikali hasara ya Tsh. Bilioni 1.16 inayomkabili Mtendaji wa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (Rahco), Benhard Tito na wenzake, wameuomba upande wa mashtaka kuondoa hati ya kuzuia dhamana ili washitakiwa wapate dhamana.

Hayo yameelezwa na Wakili wa utetezi, Melkior Sanga katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati kesi hiyo ilipoitishwa kwa ajili ya kutajwa.
Hatua hiyo inatokana na Wakili wa Serikali, Oliver Bukuru kudai kuwa jalada la kesi hiyo lipo kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) na litakapokuwa tayari Mahakama itajulishwa.
Wakili Sanga amedai kesi hiyo ni ya muda mrefu tangu March 14, 2016”Kwa sasa upelelezi umekamilika hivyo tunaomba upande wa Jamhuri waondoe hati hiyo ili wateja wetu wapate dhamana.”
Hakimu Simba alizitaka pande zote mbili utetezi na mashtaka watoe matokeo ya kesi hiyo itakapotajwa September 11, 2018.
Mbali na Tito, washitakiwa wengine ni mfanyabiashara Kanji Mwinyijuma na Katibu wa Rahco, Emmanuel Massawe ambao wanadaiwa kula njama, matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia serikali hasara ya Dola za Marekani 527,540 sawa na Tsh Bilioni 1.16.

Post a Comment

0 Comments